Zijue sababu za utumbo mkubwa kutoka nje ya sehemu ya kutolea haja kubwa kwa watoto na matibabu yake

                                                   Image result for rectal prolapse in children
MWAKA 2015, Mariam John alijifungua salama mtoto wake wa pili Elizabeth Peter (si majina yao halisi), huko mkoani Kigoma ambako ndipo yalipo makazi yao.

Maendeleo ya afya ya Elizabeth yalikuwa yanaridhisha kila walipohudhuria kliniki lakini miaka miwili baada ya kuzaliwa hali ilianza kubadilika ghafla.
Mariam anasema siku moja alipokuwa akimnawisha sehemu ya haja kubwa mtoto wake huyo, baada ya kumaliza kujisaidia alishangaa kugusa kinyama ambacho kilijitokeza kwa nje.

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa watoto Muhimbili, Zaituni  Bokhary anasema Elizabeth alipata tatizo linalojulikana kitaalamu Rectal Prolapse.

“Hii ni hali ambayo sehemu ya utumbo mkubwa iitwayo ‘rectum’ hutoka nje ya mwili katika njia ya haja kubwa. Hakuna sababu maalumu ambayo wataalamu tunaweza kusema moja kwa moja, kwamba tatizo limesababishwa ama na bakteria au wadudu. Lakini kuna viashiria au visababishi kadhaa ambavyo vinahusishwa kusababisha tatizo hilo kutokea” .

Visababishi
Hali hiyo inaweza kusababishwa na kuharisha muda mrefu hali ambayo huchangia mtoto kupungua uzito na kukonda mwili. Hii ni sababu kuu, kuharisha muda mrefu husababisha mtoto kukonda hadi ile misuli ya haja kubwa hushindwa kukaza vizuri kama inavyotakiwa hali hiyo huifanya ile ‘rectum’ kutoka nje

Kiashiria kingine cha awali ambacho mzazi anaweza kukiona iwapo mtoto anakabiliwa na tatizo hilo ni kupata viotea (vinyama) ambavyo hutoka katika njia ya haja kubwa. Vinyama hivyo hutoka nje ya mwili katika sehemu ya haja kubwa. Wakati mwingine tatizo huweza kujitokeza iwapo kuna maambukizi katika utumbo mkubwa

Iwapo mtoto aliwahi kufanyiwa upasuaji wa utumbo mkubwa, inaweza kusababisha akapatwa tatizo hilo kwa namna moja au nyingine.

Lakini wengine wanapata tatizo hili, ikiwa wamezaliwa na hawana chembe chembe maalumu ambazo kazi yake kuu ni kusukuma choo nje ya mwili, sasa kwa kuwa hajazaliwa na chembe chembe hizo mtoto huyo anaweza utumbo wake ukatoka nje kwa sababu ya kutumia nguvu kusukuma choo

Hatua za tatizo
Daktari huyo anasema ugonjwa huo hupitia hatua kuu nne na kwamba iwapo mzazi atawahi kumfikisha mwanawe hospitali matibabu yanaweza kufanyika bila kutumia njia ya upasuaji ila endapo atacheleweshwa kupatiwa matibabu kwa dalili za awali matibabu yatahiji njia ya upasuaji.

HATUA YA KWANZA
Katika hatua ya kwanza mzazi au mlezi ataona ule utumbo unatoka na kurudi ndani wenyewe, sasa anapomleta hospitali mtoto anamfanyia uchunguzi kujua nini kinasababisha hali hiyo, atatibiwa kwa kutumia dawa maalumu na wala hatahitaji kufanyiwa upasuaji wowote

HATUA YA PILI
Anataja hatua ya pili ya tatizo kuwa utumbo unapotoka nje hushindwa kurudi ndani bila kusaidiwa kuurudisha.

HATUA YA TATU
Kwa maelezo ya kidaktari “hatua ya tatu huashiria kwamba tatizo linazidi kuwa kubwa na kwamba utumbo wa mtoto huweza kujitokeza nje hata kama hakujisaidia.” Inapofikia hatua hii matibabu hufanyika kwa njia ya upasuaji.

JINSI YA KUMKINGA MTOTO
watoto wengi ni rahisi kupatwa na hali hiyo hasa wale wanaoishi katika mazingira machafu.

Inaaminika kwamba  tatizo la kuharisha maana yake amekula vitu vichafu,  watoto wanapocheza hushika vitu vingi, na wengi hupenda kuweka vidole mdomoni.

 mazingira yanapokuwa machafu mtoto anakuwa kwenye hatari zaidi ya kupata maambukizi, ni vema mazingira yakasafishwa kila wakati yawe rafiki kwa watoto ili kuwaepusha
Pindi tu uonapo dalili zilizotajwa hapo juu ni vema kwenda kwenye kituo cha afya kupata matibabu zaidi.

Post a Comment

Previous Post Next Post