Mwanza: Achanwa tumbo hadi kutolewa utumbo kwa kuhoji matumizi ya Tsh. 10,000 aliyoacha asubuh

Benedictor Gogogo (48) mkazi wa kijiji Cha Itabagumba Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza nchini Tanzania amenusurika kifo kwa kuchanwa tumbo na kitu chenye ncha kali hadi utumbo kutoka nje baada ya kutokea ugomvi kati yake na mke wake.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu leo Alhamisi Januari 2, 2020, Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Jumanne Murilo amesema tukio hilo lilitokea jana Jumatano.

“Tunamshikilia mtuhumiwa kwa mahojiano na uchunguzi zaidi kuhusu tukio hilo,” amesema Kamanda Muliro

Akisimulia tukio hilo akiwa katika wodi ya Hospitalini ya Wilaya ya Sengerema anakopata matibabu, Gogogo amesema mzozo kati yake na mke wake aliyemtaja kwa jina la Mama Asteria ulitokana na kuhoji matumizi ya Sh10,000 aliyoacha nyumbani asubuhi ya siku ya tukio.

“Wakati naondoka kwenda kwenye shughuli zangu za uvuvi, asubuhi ya siku ya tukio, niliacha Sh10,000 ya matumizi.

Niliporejea nilimwomba mama Asteria anipe Sh1,000 kati ya fedha nilizoacha ili ninunulie vocha ya simu lakini akaniambia fedha yote imeshatumika,” amesema

“Nilipohoji zaidi akaanza kunitolea majibu yaliyonikasirisha na kunifanya nimpige kofi na kutokea mzozo kati yetu ambao hata hivyo uliisha na mimi kuingia ndani kujipumzisha.”

Anasema akiwa ameanza kupitiwa usingizi, mke wake ambaye wameishi mwaka mmoja na nusu sasa alimvizia na kumchana na kitu chenye ncha kali tumboni hadi utumbo kutoka nje.

Anawashukuru majirani kwa kujitokeza kumsaidia kwa kukodisha mtumbwi na kumkimbiza hospitalini anakoendelea kutibiwa.

Mganga mkuu wa Hospitali Teule ya Wilaya ya Sengerema, Sista Mery Jose amesema hali ya mgonjwa huyo inaendelea vema na bado wamemweka chini ya uangalizi wa karibu kitabibu.

Post a Comment

Previous Post Next Post